• CHAMA CHA MAPINDUZI

    MWENYEKITI WA CCM, RAIS JAKAYA KIKWETE AKIWA NA WAJUMBE WA NEC, 25/9/2012, KABLA YA KIKAO KILICHOFANYIKA MJINI DODOMA, KUTEUA WAGOMBEA WA NAFASI MBALIMBALI ZA UONGOZI NDANI YA CHAMA. PICHA: BASHIR NKOROMO
  • CHAMA CHA MAPINDUZI

    CCM NDICHO CHAMA CHA SIASA KINACHOONGOZA KWA KUWA NA WAFUASI WENGI TANZANIA
  • CHAMA CHA MAPINDUZI

    CCM CHAMA MAKINI KINACHOFANYA MAAMUZI KWA VIKAO RASMI
  • CHAMA CHA MAPINDUZI

    MWENYEKITI WA CCM, RAIS JAKAYA KIKWETE AKIWA NA WAJUMBE WA NEC, 25/9/2012, KABLA YA KIKAO KILICHOFANYIKA MJINI DODOMA, KUTEUA WAGOMBEA WA NAFASI MBALIMBALI ZA UONGOZI NDANI YA CHAMA. PICHA: BASHIR NKOROMO
  • CHAMA CHA MAPINDUZI

    CCM NDICHO CHAMA CHA SIASA KINACHOONGOZA KWA KUWA NA WAFUASI WENGI TANZANIA

Vurugu zilizofanywa Dar, Z’bar ni siasa za kuelekea mwaka 2015?


Na Charles Charles

JUMATANO iliyopita, Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Kondo Bungo, alinukuliwa na gazeti moja la kila siku nchini, akitangaza kufanyika kwa maandamano makubwa nchi nzima wiki hii, kushinikiza kuachiliwa huru kwa Katibu wa Jumuiya hiyo, Sheikh Ponda Issa Ponda na wenzake waliofunguliwa kesi mahakamani.

Wito wa Sheikh Kondo ulikuja siku tatu tu baada ya Wajumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Profesa Abdallah Safari na Mabere Nyaucho Marando, kutangaza kuyaunga mkono maandamano yote ya vurugu yaliyofanywa na watu wanaodaiwa kuwa wafuasi wa Sheikh Ponda, Tanzania Bara, na wafuasi wa Jumuiya ya Mihadhara ya Kiislamu (Uamsho), kwa Zanzibar.

Aidha, chama cha Civic United Front (CUF) kupitia kwa Mwenyekiti wa Taifa, Profesa Ibrahim Haruna Lipumba nacho kilijitokeza hadharani, siku moja baada ya kauli ya Sheikh Kondo, kutaka Sheikh Ponda na wafuasi wake walioshtakiwa Oktoba 18, waachiliwe huru na kusema kuwa kitendo cha serikali cha kupeleka Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kutaka kupambana na waandamanaji “ni cha aibu na kinasikitisha”.

Tayari Baraza la Maaskofu wa Makanisa ya Kipentekoste Tanzania (PCT), limeomba radhi kwa waislamu wote nchini walioguswa kwa namna moja ama nyingine na kukojolewa kwa Kitabu Kitukufu cha Kur’ani, kitendo kilichofanywa Oktoba 12, mwaka huu, na mtoto wa Shule ya Sekondari ya Nzasa jijini Dar es Salaam.

Kufuatia maandamano ya vurugu yaliyofanywa na watu wanaoaminika kuwa ni waislamu, kwanza huko Mbagala, Oktoba 12, kupinga kudhalilishwa kwa kitabu hicho cha dini yao na kutaka wakabidhiwe mtoto huyo ili wamchinje hadharani.

Siku chache baadaye ilipofika Oktoba 20, wafuasi wa Sheikh Ponda anayekabiliwa na kesi ya jinai katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, nao waliandamana, kushinikiza aachiliwe huru yeye na wafuasi wake anaoshtakiwa nao kwa tuhuma nyingine za jinai. Hapo ndipo serikali ikatuma takribani kombania tatu za JWTZ ili zisaidiane na askari wa Jeshi la Polisi kukabiliana na wafanya fujo hao.

Kesho yake, serikali kupitia kwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel John Nchimbi ndipo ikasema kwamba walioshiriki katika vitendo hivyo vyote ni wahuni tu.

Alikuwa akimaanisha sababu za kuandamana kwao huku wakifanya vurugu, kuyavamia makanisa na kuyavunja, wakaiba mikate ya meza ya Bwana na divai zake, wakachoma Biblia, kukojolea madhabahu, kuiba kwenye maduka ya watu, kusababisha kufungwa kwa shughuli zote katikati ya jiji na uhalifu mwingine kwamba hakuhusiani chochote na msingi wowote ule wa kidini.

Alimaanisha kwamba huo ni uhalifu kama mwingine wowote ule wa jinai. Hautokani na agizo wala kitabu cha dini yoyote, hivyo hawawezi kusingizia kwamba walifanya hivyo ili kutetea haki, hadhi wala sheria za dini yoyote bali ni wahuni wanaotaka kuutumia uislamu kuwa kichaka cha kufichia uhalifu wao.

Pamoja na ukweli huo wote, kauli hiyo ya Nchimbi bado imeonyesha kutokubaliwa na PCT kupitia taarifa yake iliyosomwa kwa waandishi wa habari na mmoja kati wa wajumbe wake, Dk. Mgulu Kilimba.

“Kauli hiyo inamaanisha kuwa serikali haiamini kuwa waliohusika na uvunjaji wa makanisa, kuchoma (moto) Biblia, kubomoa na kukojolea madhabahu, kunywa na kula mikate ya meza ya Bwana na hatimaye kuwapiga watumishi wa Mungu ni wanaharakati wa kidini”, inasema taarifa hiyo.

Nimefuatilia kwa muda mrefu sakata hili zima lilipoanza kwa mtoto yule kuikojolea Kur’ani na kusababisha maandamano yale ya ghasia, uporaji ukiwemo wa kutumia nguvu, uvunjaji wa makanisa, uchomaji moto Biblia, kukojolea madhabahu kanisani mpaka maandamano ya pili yaliyodhibitiwa kikamilifu, katikati ya jiji hilo la Dar es Salaam.

Nimeziangalia hoja na madai yanayotolewa na watu mbalimbali wakiwemo wanasiasa kama akina Profesa Abdallah Safari, Mabere Marando, Profesa Ibrahim Lipumba, Sheikh Kondo Bungo na hatimaye PCT mbali na ubishi unaotokea mitaani na sehemu nyingine hasa zenye mikusanyiko ya watu wa kada na fani tofauti.

Wengi kati yao hawakubaliani moja kwa moja na maandamano yote yaliyofanywa kuanzia ya Mbagala hadi ya Oktoba 17 huko Zanzibar na hata yaliyodhibitiwa na polisi katika mitaa ya Kariakoo, Magomeni, Mnazi Mmoja na maeneo mengine jijini Dar es Salaam, siku mbili baadaye.

Hawakubaliani nayo kwa sababu yanaonekana kwamba yalifanyika kwa kupangwa na hivyo madai yaliyotolewa na wahusika ambayo yamekuja kushadidiwa na watu kama akina Safari, Marando, Lipumba na Sheikh Kondo ni visingizio vinavyolenga kuficha malengo halisi.

Pamoja na kutofungamana na upande wowote kati ya zote zinazovutana, lakini nakubaliana na wale wanaolaani mikakati na kauli zote zinazounga mkono uovu huo. Nakubaliana nao maana hakuna ubishi kwamba hata kwa sheria zote duniani, mtu yeyote mwenye umri wa chini ya miaka 18 bado ni mtoto.

Anachukuliwa kuwa hawezi kuchanganua jema au jambo lolote ambalo ni baya kwa vile hajui lolote wala chochote maana ni mtoto na hivyo akili zake pia ni changa.

Ndivyo ilivyokuwa kwa mtoto huyo wa Mbagala aliyekojolea Kur’ani. Hakufanya hivyo kwa makusudia ama nia yoyote ile kwa waislamu na uislamu kama dini. Ndiyo maana pia inaelezwa kuwa alikikojolea kitabu hicho ili kuona kama vitisho alivyokuwa akitishiwa na mwenzake vina ukweli au vilikuwa hadithi za alinacha.

Kama inavyofahamika dunia nzima, hakuna watu wanaopenda sana kujaribu kitu chochote kama watoto. Ndiyo maana wataalamu wanaeleza wazi kuwa mtoto ndiye binadamu ambaye ana uwezo mkubwa zaidi wa kukariri mambo au kufanya majaribio mpaka aridhike.

Anapenda kuthibitisha kila jambo analosikia, kuambiwa au kuhadithiwa kwa kutaka kuona kwa macho yake mwenyewe, kushika au kugusa kwa mikono yake, kuonja kwa ulimi wake, kuongelesha kwa kinywa chake na kadhalika. Hawezi kuambiwa kitu na hasa anachodhani kuwa kinasisimua sana, kushangaza au kuringishia halafu akaitikia mdomoni kwa urahisi na kuishia hapo.

Ni lazima asikilize kwa makini yake yote, abishane sana, aulize maswali, adadisi takribani kila kipengele au ufafanuzi anaopewa na hata vinginevyo.

Ndivyo ilivyokuwa pia kwa mtoto aliyekojolea Kur’ani ambapo kuna watu wanadai kuwa aliambiwa kama angefanya hivyo angegeuka chatu palepale, mbuzi ama angekumbwa na kichaa cha akili papo hapo.

Kwa vile hakuamini vitisho hivyo na kusema haiwezekani huku mwenzake akisisitiza kuwa ni kweli, mtoto huyo aliamua akate mzizi wa fitina kwa kuiweka chini, akaikojolea na kisha akabaki ni binadamu yuleyule, vilevile na palepale wala hakugeuka chatu, mbuzi au kupata wendawazimu wa akili na hata vinginevyo.

Siyasemi haya kwa kuangalia jina langu kuwa ni mkristo kwa sababu kama ni dini ninatoka kwenye familia ya kikristu na kiislamu. Wakati baba yangu ni mkristu, marehemu mama yangu mzazi na marehemu dada yangu walikuwa waislamu na mimi pia nilianzia katika dini hiyo kabla sijaamua rasmi kufuata imani ya baba.

Hadi hivi leo kwa mfano ukienda nilipokulia pale Temeke Mikoroshini, Dar es Salaam, au kijijini kwetu na katika ukoo wote wa mama unitafute kwa kutumia jina hili kuna wengine watasema hawanifahamu.

Hiyo ni kwa sababu wamezoea jina lile jingine nililokua nalo, lakini hatimaye likayeyuka polepole na kutoweka miongoni mwao. Wakaingiwa na hili la pili walilokuja kulifahamu rasmi nilipokuwa nasoma shule, lakini lilishika kasi zaidi nilipoacha jeshi katika JWTZ na kuanza kazi hii ya uandishi wa habari magazetini.

Najiuliza pia kuhusu madai kuwa mtoto yule alitumwa na baadhi ya watu amdanganye mwenzake kwamba kama angeikojolea Kur’ani angegeuka chatu, mbuzi ama angepata wendawazimu papo hapo.

Walitaka wafanye hivyo ili kukidhi matakwa yao ya kisiasa au ya kiuchumi ikiwemo kuiba, kuvunja makanisa na kuwapiga watumishi wake, kuchoma moto Biblia na kufanya uhalifu mwingine.

Najiuliza kama kweli ni mpango uliosukwa na kundi la wahalifu wa kawaida mitaani, lakini ili kuvichanganya vyombo vya dola wakamtumia mtoto huyo wa kiislamu amshawishi kwa kutumia vitisho mtoto wa kikristu ili ashawishike kirahisi kuikojolea Kur’ani, hatua ambayo ingewapa nafasi na sababu za kuanzishia vurugu na kukidhi matakwa yao yote.

Walijua kitendo hicho kingewachukiza waislamu katika upande wa kwanza, na pia walijua wasingeweza kukivumilia, hivyo wangeutumia mwanya huo kama kisingizio cha kuanzishia vurugu ili kutimiza matakwa yao yakiwemo yaliyotajwa na viongozi wa PCT wiki iliyopita.

Kama ni kweli kuwa kosa lile lilifanywa na mtoto yule ili kuudhalilisha uislamu, kwa nini wakristu hawakuandamana popote, wakafanya ghasia, wakavunja misikiti, kuchoma moto Kur’ani, kukojolea kibra misikitini wala kuwapiga masheikh au maimamu ili kulipa kisasi cha uhalifu waliofanyiwa kule Mbagala?

Au, nani aliyefanya kosa kubwa zaidi kati ya mtoto aliyekojolea Kur’ani bila kujua kuwa ni kosa kwa kuzingatia umri wake na watu wazima waliovamia makanisa na kuyavunjavunja, wakaiba divai na mikate ya meza ya Bwana, kuzichoma moto Biblia, kukojolea madhabahu ya kuongozea ibada au kuwapiga watumishi wake na kadhalika?

Hadi hapo kwa nini nisiamini kuwa hayo yaliyofanywa au yanayofanywa ama kuchochewa na viongozi kama akina Profesa Abdallah Safari, Profesa Ibrahim Haruna Lipumba, Mabere Nyaucho Marando, Sheikh Kondo Bungo na wengineo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango mzito wa siri walionao dhidi ya Serikali ya Awamu ya Nne?

Kwa nini nisiamini kuwa wanafanya hivyo ili kutimiza kilichosemwa na baadhi ya vyama vya siasa pindi tu baada ya kushindwa uchaguzi mkuu wa rais, wabunge na madiwani wa mwaka 2010 kwamba watahakikisha Tanzania haitawaliki katika kipindi hiki cha kuelekea mwaka 2015?

Mwandishi wa makala hii ni Katibu Msaidizi, Idara ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa ya CCM. Anapatikana kwa Simu Na. 0659 220 220 na 0762 633 244

This entry was posted in

Leave a Reply