• CHAMA CHA MAPINDUZI

    MWENYEKITI WA CCM, RAIS JAKAYA KIKWETE AKIWA NA WAJUMBE WA NEC, 25/9/2012, KABLA YA KIKAO KILICHOFANYIKA MJINI DODOMA, KUTEUA WAGOMBEA WA NAFASI MBALIMBALI ZA UONGOZI NDANI YA CHAMA. PICHA: BASHIR NKOROMO
  • CHAMA CHA MAPINDUZI

    CCM NDICHO CHAMA CHA SIASA KINACHOONGOZA KWA KUWA NA WAFUASI WENGI TANZANIA
  • CHAMA CHA MAPINDUZI

    CCM CHAMA MAKINI KINACHOFANYA MAAMUZI KWA VIKAO RASMI
  • CHAMA CHA MAPINDUZI

    MWENYEKITI WA CCM, RAIS JAKAYA KIKWETE AKIWA NA WAJUMBE WA NEC, 25/9/2012, KABLA YA KIKAO KILICHOFANYIKA MJINI DODOMA, KUTEUA WAGOMBEA WA NAFASI MBALIMBALI ZA UONGOZI NDANI YA CHAMA. PICHA: BASHIR NKOROMO
  • CHAMA CHA MAPINDUZI

    CCM NDICHO CHAMA CHA SIASA KINACHOONGOZA KWA KUWA NA WAFUASI WENGI TANZANIA

Hakuna kitakachoshindikana CCM bila ya mabinti wa Wassira kuwepo


Na Charles Charles

KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Wilbroad Slaa aliwafanyia tafrija maalum ikiwemo kuwaitia waandishi wa habari, mabinti wawili wa kaka wa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Stephen Wassira walipokwenda kuchukua kadi za chama chake.

Tukio hilo ambalo lilitokea Septemba 29, lilifanyika Makao Makuu ya Chadema jijini Dar es Salaam ambapo Dk. Slaa aliwatumia kama mtaji wa kisiasa, akiwataka Watanzania wengine pia waachane na Chama Cha Mapinduzi (CCM) “ili kuleta mabadiliko” nchini.

Wanawake hao ni Lilian na Esther George Wassira na katika hotuba yake kwao, Dk. Slaa alimshutumu baba yao mdogo kwamba ni “kinara wa kuuaminisha umma kuwa wanaodai hali bora ya maisha kwa Watanzania ni wenye vurugu”, lakini hafahamu endapo “maisha yakiboreka hata wengine katika familia yake (mwenyewe nao) watayafurahia”.

Sitaki niamini kuwa Dk. Slaa kama msomi wa falsafa ya teolojia, mbunge wa zamani, mgombea urais aliyeshindwa, Katibu Mkuu wa chama cha siasa kinachojipa hadhi ya upinzani mkuu kwa serikali na padri wa zamani kumbe ana upeo mfupi kiasi hicho!

Sikutarajia kama angewaona wanawake hao ni muhimu zaidi kuliko wanachama na viongozi wengine wa Chadema akiwemo yeye, wale ambao kila mmoja alihamia katika chama hicho kwa muda wake na sababu anazozijua mwenyewe.

Anawaona muhimu kuliko Makamu Mwenyekiti wa Chadema (Tanzania Bara), Said Amour Arfi aliyetokea CCM mwaka 2005; Makamu Mwenyekiti (Zanzibar), Saidi Issa Mzee; Mkurugenzi wa Fedha na Utawala, Anthony Komu na Mkuu wa Kitengo cha Intelijensia, Mabere Nyaucho Marando waliohamia huko wakitokea NCCR – Mageuzi; Mkurugenzi wa Kampeni na Uchaguzi, Msafiri Abdulrahman bin Salim wa Mtemelwa aliyetoka Chama Cha Wananchi (CUF) na kadhalika!

Ibara ya 3(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 Toleo la 2005 inasema “Jamhuri ya Muungano ni nchi ya kidemokrasia na ya kijamaa, isiyokuwa na dini na yenye kufuata mfumo wa vyama vingi vya siasa”.

Katika hali hiyo, Mtanzania yeyote asiyepungua miaka 18 ana haki ya kujiunga na chama chochote kile cha siasa, hivyo inashangaza kumuona Dk. Slaa akiingia wendawazimu baada ya wanawake hao wawili kujiunga Chadema.

Nashangaa kwa sababu hawana historia wala rekodi yenye tija kwa chama chochote kile cha siasa, na pia hakuna kumbukumbu inayoonyesha kwamba walifanya jambo kubwa lolote na mahali popote iwe nyumbani, shuleni au chuoni na hivyo kwenda kwao Chadema ni hatua ambayo itakiletea chama hicho faida ya maana kisiasa dhidi ya vyama vingine.

Kama alivyosema Waziri Stephen Wassira kesho yake alipokutana na waandishi wa habari mjini Bunda mkoani Mara, Lilian na Esther ni akina mama wa nyumbani na wafanyakazi wa kawaida wakiwa wanasheria, hivyo hakuna faida yoyote kwao kuingia Chadema wala pengo lolote waliloacha katika familia ama ukoo wao kwa hatua yao hiyo.

Kama kungekuwa na rekodi au historia yoyote kwamba walipokuwa CCM au chama kingine chochote kile cha siasa walifanya jambo fulani kubwa, lile ambalo bila wao lisingewezekana na hivyo kuhama kwao ni pigo walikotoka hapo ingekuwa kweli kuwa Chadema ‘imelamba dume’.

Lakini kwa sababu hakuna rekodi hiyo, nalazimika kuamini kwamba Dk. Slaa na Chadema yake wanataka kuwafanya kuwa mtaji wa kisiasa siyo kwa kupitia majina yao kama Lilian na Esther George isipokuwa baba yao mdogo, Stephen Wassira.

Wanataka kuwadanganya Watanzania kuwa ni watoto wake halisi na mkewe, ukweli ulioanza kuonekana wakati Katibu Mkuu huyo wa Chadema alipoita waandishi wa habari na kufanya tafrija ya kuwapokea, wakapigwa picha na kutangazwa kwenye televisheni pamoja na magazeti kwamba wanatoka familia ya waziri huyo, kiongozi ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM.

“Ndugu yangu Wassira amekuwa kinara wa kuuaminisha umma kuwa wanaodai hali bora ya maisha kwa Watanzania ni wenye vurugu pasipo kujua maisha yakiboreka hata wengine katika familia yake mwenyewe watanufaika”, alisema ili kuonyesha uongo wake kwamba wanawake hao “wamekiasi chama cha baba yao ingawa ni waziri” na kisha wakakimbilia Chadema.

Anataka kuwadanganya Watanzania kuwa chama hicho kina sera nzuri, kinatetea wananchi na kupigania maisha bora kwa wote na ndiyo maana sasa kinakimbiliwa hadi na watoto wa viongozi waandamizi wa CCM na serikali yake.

Aliita waandishi wa habari na kuwafanyia tafrija maalum siyo kwa sababu anawapenda sana au wana kitu cha ziada kuliko Said Amour Arfi, Anthony Komu, Msafiri Mtemelwa, Mabere Marando; Mkurugenzi wa Sera na Utafiti, Mwita Waitara; Mkurugenzi wa Organaizesheni, Benson Kigaila na hata Wajumbe wa Kamati Kuu akina Profesa Abdallah Safari na Profesa Mwesiga Baregu ambao pia walikwenda Chadema wakitokea vyama vingine.

Alilenga kuwafanya akina mama hao kwamba ni muhimu kuliko jopo hilo lote na ndiyo maana hakuna aliyepewa mapokezi hayo maalum kama wao, hivyo kwenda kwao Chadema kutakifanya chama hicho kiwe juu zaidi kisiasa kushinda wakati wote mwingine kabla yao.

Hata hivyo, kamwe sioni faida yoyote ya kisiasa kwa Chadema kutokana na hatua yao hiyo zaidi ya kuongeza orodha ya wanachama wanawake, na pia hakuna hasara na hata pengo lolote itakalopata CCM endapo wamewahi kuwa wanachama wake ama familia ya Waziri Stephen Wassira ambako kwanza hawatoki.

Mwaka 1995, mtoto wa kiume wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Kapteni Makongoro Kambarage Nyerere aliingia NCCR – Mageuzi ambako aligombea ubunge wa Arusha Mjini na kushinda, lakini CCM haikuyumba wala kutikisika kwa namna yoyote ile eti kwa sababu aliihama na kujiunga na upinzani.

Alidumu katika chama hicho kwa miaka takribani sita na kurejea CCM, hatua ambayo hata Waziri Wassira naye amewahi kuifanya alipohamia katika chama hicho mwaka uleule wa 1995 pamoja na Makongoro, lakini akarejea alipogundua kuwa upinzani ni kama jukwaa la ‘ze komedi’.

Katika hali hiyo, hata watoto hao wa kaka yake waziri huyo huenda wakaondoka Chadema na kuingia chama kingine, kile ambacho kinaweza kuwa CCM ama vinginevyo, lakini hata iweje hakuna faida yoyote itakayopatikana ya kwenda kwao huko.

Hawawezi kufananishwa kwa namna yoyote ile kisiasa na watu kama Profesa Abdallah Safari, Profesa Mwesiga Baregu, Said Amour Arfi, Saidi Issa Mzee, Mabere Nyaucho Marando, Msafiri Mtemelwa, Mwita Mwikwabe Waitara, Benson Kigaila, Anthony Komu wala Mkurugenzi wa Idara ya Ulinzi ya Chadema ambaye pia ni mbunge wa zamani wa Bukoba Mjini kupitia CUF, Wilfred Lwakatare.

Hawawezi kuwa lolote kisiasa kuliko viongozi hao akiwemo mbunge wa sasa wa jimbo la Kigoma Kusini (NCCR – Mageuzi), David Kafulila aliyefananishwa na sisimizi kwa kauli iliyotolewa na Dk. Slaa mwenyewe wa waandishi wa habari mwaka 2009.

Alikashfiwa kwa maneno yote ‘machafu’, kejeli na dharau kwa sababu tu alimuunga mkono Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Zuberi Kabwe wakati wa kinyang’anyiro cha kuwania nafasi ya Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema.

Alionekana hatari kwa sababu tu alikuwa Meneja wa Kampeni za Zitto ambaye naye alishinikizwa ajiuzulu katika mbio hizo ili amuache Freeman Mbowe awe mgombea pekee, mfumo ambao haupo katika chama hicho bali uliletwa ili kukidhi matakwa ya ukabila, udini na ukanda.

Siwadharau wala kuwakejeli wanawake hao kwa hatua yao hiyo ya kwenda Chadema, lakini sikubaliani na juhudi za kutumia nafasi ya baba yao mdogo serikalini kutaka kuwapandisha chati ili waonekane muhimu, na pia hakuna jambo lolote litakaloshindikana kufanyika katika CCM eti kwa vile mabinti hao sasa hawapo.

Mwandishi wa makala hii ni Katibu Msaidizi, Idara ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa ya CCM. Anapatikana kwa Simu Na. 0659 220 220 na 0762 633 244

This entry was posted in

Leave a Reply