WANAOKWENDA CHADEMA AMA NI WAPAMBE WA LOWASSA AMA WAMESHINDWA KURA ZA MAONI
Na Charles Charles SITAKI kumjadili mtu mwingine yeyote aliyekikimbia Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kuhamia Chama cha Demokrasia na Mae... [Read More]
Na Charles Charles SITAKI kumjadili mtu mwingine yeyote aliyekikimbia Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kuhamia Chama cha Demokrasia na Mae... [Read More]
Na Charles Charles IPOKUWA katika ziara zake za kutafuta wadhamini 200 ili kukidhi matakwa ya kisheria, mgombea wa kiti cha Rais wa J... [Read More]
owassa aliyekuwa fisadi akiwa CCM hata Chadema ni yuleyule Na Charles Charles JUMAPILI iliyopita, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasi... [Read More]
Na Charles Charles
IJUMAA iliyopita, wabunge wote wa kambi ya upinzani katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania waliokuwa kwenye kikao cha nne cha mkutano unaoendelea sasa mjini Dodoma, walitoka nje ya ukumbi na kwenda kuongea na waandishi wa habari kwa dakika 38.
“Tumewaita kuzungumzia sababu za kutoka nje na hatua za kuchukua. Kama mlivyosikia, (James) Mbatia (ambaye ni Mbunge wa Kuteuliwa anayetoka NCCR – Mageuzi) alisema hakuna mitaala na (wala) haijawahi kuwepo tangu mwaka 1961 na kama ipo atajiuzulu”, alisema aliyekuwa mwenyekiti wa kikao hicho na Mbunge wa Singida Mashariki kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu.
Alidai kuwa Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa alisema uongo bungeni kwamba wizara yake ina mitaala ya masomo kwa shule za sekondari na msingi, lakini akashindwa kuitoa.
“…Tutapeleka taarifa ya kikao chetu katika Kamati ya Bunge ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge kumtaka Waziri Kawambwa ajiuzulu kwa kulidanganya bunge, ikishindikana tutaipeleka tena katika mamlaka zilizomteua”, alibainisha.
Aliongeza kuwa endapo mamlaka hiyo pia haitamwajibisha, wabunge hao watapiga kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ili kuilazimisha serikali nzima ijiuzulu, hatua itakayomfanya Rais Jakaya Kikwete ateue baraza jipya la mawaziri kama ilivyokuwa Februari 6, 2008 wakati aliyekuwa Waziri Mkuu wakati huo, Edward Lowassa alipoamua kujiuzulu kwa kuwajibika kisiasa.
Mbali na kufanya hivyo dhidi ya Pinda, wabunge hao waliwaambia waandishi wa habari kwamba wataandaa hoja nyingine ya kuwang’oa Spika wa Bunge, Anne Makinda na Naibu Spika, Job Ndugai kwa tuhuma za kukandamiza hoja zao.
“Tulitaka kujadili hoja ya gesi ya Mtwara, lakini Spika akaizima, akasema itaundwa tume, baadaye tume hakuna baada ya Waziri Mkuu kwenda (huko). Tangu Mbatia awasilishe pia hoja yake inaonyesha waziwazi (kwamba nayo) wanataka kuizima”, alisema Tundu Lissu ambaye pia ni Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani katika bunge hilo la 10.
Nasema siyo lazima mtu awe mpaka mwanasheria, daktari wa falsafa au profesa wa fani yoyote ndipo aweze kuuona ujinga unaofanywa na kambi hiyo ya upinzani isipokuwa hata akisoma kwa kawaida.
Haiwezekani kwamba serikali bado haina mitaala ya elimu nchini tangu nchi yetu ipate Uhuru wake mwaka 1961 hadi leo, madai ambayo ni uongo uliovuka mpaka na kuwa ni uzandiki unaotia ukakasi hata kuuzungumza mdomoni.
Ingawa ni kweli kuwa mimi siyo mwalimu na kamwe sikusudii kufanya kazi hiyo hata siku moja hapo baadaye, lakini najua mitaala ya masomo kwa shule za msingi na sekondari hapa nchini ipo, hivyo anayesema vinginevyo ingekuwa bora kama angetuambia kwamba anayodai yeye imechelewa kuanza na kueleza imechapishwa lini ili umma ufahamu.
Nilipokuwa nasoma mwaka ule wa mwisho wa elimu yangu ya msingi nilichukuliwa na mjomba wangu aliyekuwa mwalimu mkuu shuleni kwetu, hivyo nilikuwa naziona nakala za mitaala hiyo ambayo haikuwa ya mwaka 1960, 1959 au 1958 ya kabla ya Uhuru kwa sababu hata marehemu mama yangu mzazi alikuwa bado ni mtoto wa miaka 11 tu wakati Tanzania Bara inajitawala hapo Desemba 9, 1961.
Nilikuwa naishi palepale shuleni na mjomba wangu huyo na baadhi ya walimu, hivyo nilikuwa pia naona wakiandaa masomo ya kwenda kutufundisha madarasani siyo kwa matakwa yao wenyewe, bali walitumia mitaala hiyo ya elimu inayotungwa serikalini.
Mbatia aliyeshindwa kukijenga chama chake ambacho yeye ndiye Mwenyekiti wa Taifa anadhani atakijenga kwa kuwasilisha hoja hizo za uongo na uzushi bungeni.
Anadhani kwa kufanya hivyo kitafufuka tena kama ilivyokuwa Februari 28, 1995, siku ambayo aliyewahi kuwa Naibu Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Augustine Lyatonga Mrema alipohamia huko akitokea Chama Cha Mapinduzi (CCM) kutokana na uchu wake wa kutaka kugombea urais.
Anadhani kitafufuka na kuwa na nguvu kiliyodumu nayo kuanzia hapo hadi mchana wa Jumapili Aprili 25, 1999, siku ambayo Mrema alitangaza ghafla tena kuachana na chama hicho na kuhamia Tanzania Labour Party (TLP) na kusambaratika nchi nzima siku ileile.
Endapo anatumia hoja hiyo akidhani itamjenga kisiasa au chama chake basi aelewe kuwa amedanganywa kama mtoto anayesoma shule ya chekechea. Ni vizuri akimshukuru Rais Jakaya Kikwete kwa kumteua kushika nafasi hiyo, ile ambayo alijitosa kuigombea mwaka 2010 katika jimbo la Kawe jijini Dar es Salaam na kushindwa vibaya.
Anapaswa ajue kwamba hakuteuliwe ili akafanye utapeli wa kisiasa bungeni, ule ambao ni pamoja na kudai Tanzania haijawahi kuwa na mitaala katika shule za msingi na sekondari tangu ipate Uhuru wake mwaka 1961!
Aliteuliwe kuwa mbunge ili kukidhi matakwa ya Ibara ya 66(e) na 67(a) na (c) za Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 Toleo la 2005 inayotumika sasa.
Hakuteuliwa kwenda kutumia nafasi hiyo ili kusema uongo, uzushi, umbeya wala kufanya uchochezi wowote au uchonganishi kati ya Watanzania na serikali ya nchi yao.
Haiwezekani kwamba eti Waziri wa Elimu awe anazunguka na mzigo wa nakala za mitaala ya shule kila anakokwenda iwe bungeni, ndani ya vikao vya kiserikali ama pale anaposafiri kikazi nje ya nchi ili kama atatakiwa kuzungumzia suala hilo anazionyesha papo kwa papo.
Kama alivyosema hata Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, serikali katika kikao kilichopita iliahidi kuwasilisha mitaala hiyo katika kikao hiki cha sasa na kuhoji: “Sasa wasiwasi wa mbunge (Mbatia) ni nini? Tutaileta hata siku ya mwisho ya bunge”.
Tayari serikali imewasilishwa bungeni jana, Jumatano ambapo kila mbunge anatakiwa kupata nakala yake mwenyewe.
Sipendi kuamini kuwa Mbatia, Tundu Lissu, Mrema na wabunge wengine wote waliotoka nje ya bunge, Ijumaa iliyopita ni kama watoto wa chekechea katika kuchanganua mambo. Sitaki kabisa niamini kwamba akili yao bado nyembamba wakati wote wana umri wa zaidi ya miaka 18.
Mchukulie Mrema kwa mfano ambaye kama asingekimbilia bungeni angekuwa tayari ni mtumishi mstaafu wa umma kwa vile miaka yake duniani iko kwenye 70. Leo naye eti anaunga mkono upuuzi wa vijana kama Mbatia aliyezaliwa mwaka 1964 na Tundu Lissu aliyezaliwa mwaka 1968!
Kuhusu hoja ile ya kutaka Waziri Kawambwa ajiuzulu na asipofanya hivyo watapiga kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mizengo Pinda nasema lengo hilo pia ni ulevi wa madaraka waliyopewa ya uwakilishi wa wananchi bungeni.
Wandhani kuwa kwao ni wabunge basi wana akili kuliko wananchi wengine. Wanafikiri wanajua mambo mengi zaidi kuliko wote wasiokuwa wabunge, ujinga ambao mtu yeyote akiamini hivyo huwa ni mwenzawazimu kichwani.
Nakubaliana kwa asilimia 100 kuwa bunge linaweza kupiga kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu kama inavyobainishwa katika Ibara ya 53A(1) ya Katiba ya nchi inayosema:
“Bila kuathiri masharti ya ibara ya 51 ya Katiba hii, bunge linaweza kupitisha azimio la kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu endapo itatolewa hoja (ya) kupendekeza hivyo na ikapitishwa kwa mujibu wa masharti ya ibara hii”.
Hata hivyo, Ibara ya 53A(2) ya Katiba ileile inasema bila ya kuathiri masharti mengineyo ya ibara hiyo, hoja yoyote ya kutaka kupitisha kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu bado haiwezi kutolewa endapo ina mapungufu yafuatayo:
(a) Haina uhusiano wowote na utekelezaji wa majukumu ya Waziri Mkuu kwa mujibu wa Ibara ya 52 ya Katiba, na pia kama hakuna madai kwamba amevunja Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma;
(b) Haijapita miezi sita tangu alipoteuliwa kushika wadhifa huo;
(c) Haijapita miezi tisa tangu hoja hiyo pia itolewe bungeni na kukwama kupitishwa na wabunge walio wengi.
Kana kwamba haitoshi, Ibara ya 53A(3) inasema hoja ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu bado haiwezi kupitishwa bungeni isipokuwa kama itakidhi mambo yafuatayo:
(a) Itatolewa taarifa ya maandishi kwa Spika iliyotiwa saini na kuungwa mkono na wabunge wasiopungua asilimia 20 ya wote, lakini isipungue angalau siku 14 kabla ya siku iliyokusudiwa kuwasilishwa bungeni;
(b) Spika atajiridhisha kuwa masharti ya Katiba kwa ajili ya kuwasilishwa kwa hoja hiyo bungeni yote yametimizwa.
Pamoja na hayo, Ibara ya 53A(4) inasema hoja iliyotimiza masharti hayo itawasilishwa bungeni mapema iwezekanavyo na halafu mwisho; kifungu kidogo cha tano kinaeleza: “Hoja ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu itapitishwa tu iwapo inaungwa mkono na wabunge walio wengi” (mwisho wa kunukuu).
Naomba ieleweke kuwa sisemi genge hilo la kina Tundu Lissu, James Mbatia, Augustine Mrema na wenzao haliwezi kujaribu kukidhi matakwa ya Ibara ya 53A(3)(a) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania niliyoitaja.
Najua litahangaika kutaka kufanya hivyo ili kusaka umaarufu kwa Watanzania wasiojua lolote wala chochote. Litajaribu kuwarubuni wale wasiojua ukweli likitaka wadanganyike kuwa linapigania haki zao, lakini linachotafuta hasa ni sifa tu za uongo, uzushi na malengo ya siasa za kitapeli.
Haiwezekani kwamba serikali iwe inahangaikia kujibu uzushi unaotengenezwa na kikundi cha wabunge wachache wenye uchu wao wa madaraka, wale ambao wametumwa kwenda kuwasemea wananchi bungeni kwa masuala ya kweli na siyo kutunga umbeya na uzandiki.
Hakuna mpiga kura aliyewatuma kwenda kumng’oa Waziri Mkuu au kushinikiza Waziri wa Elimu kuwa lazima ajiuzulu. Waliapa kuwatumikia Watanzania wote kwa uaminifu ambao ni pamoja na Mizengo Pinda, Dk. Kawambwa na wengineo na kamwe hakuna hata mmoja aliyeagiza kwamba wakifika bungeni kazi yao kubwa iwe ni kutoka nje ya vikao.
Hakuna mwananchi aliyewatuma wakalazimishe kuwa hoja zao hata kama za uongo na uzushi ni lazima zitekelezwe kwa jinsi wanavyotaka wao, na kwamba zikipingwa ama kutolewa majibu na serikali basi iwe ni nongwa na kususia kama watoto wenye gubu kwa mama wa kambo.
Shinikizo la kutaka kuwang’oa mawaziri fulani kila wanapokwenda bungeni ni siasa zilizotengenezwa kwa chuki na wivu. Haiwezekani nchi yetu iwe na utamaduni kwamba kila kikao cha bunge akang’olewe waziri mmoja, wawili, watatu ama vinginevyo na pale inaposhindikana basi anatishiwa Waziri Mkuu.
Katika kikao kile cha Aprili, 2012, wabunge hao wa upinzani walijiorodhesha majina wakiongozwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe wakitaka eti Waziri Mkuu Pinda ang’oke madarakani.
Walifanya hivyo wakishinikiza kuondolewa kwa mawaziri sita ambao kwanza; Kamati ya Wabunge Wote wa CCM ilishauri kuwa wawajibishwe kisiasa siyo kwa sababu walifanya kosa lolote, jambo ambalo halina tatizo katika uongozi na utendaji serikalini.
Alipopata taarifa hizo kutoka kwa rafiki zake ambao ni baadhi ya wabunge wa CCM, Zitto alitaka palepale kuwa mawaziri hao wang’olewe “mara moja” utadhani wahalifu wa jinai. Akasema wasipotoka basi wapinzani wangepiga kura ya kukosa imani na Waziri Mkuu na hivyo yeye ndiye abebe msalaba wao.
Licha ya kuanza kujiorodhesha majina kwa mbunge huyo mwenyewe kukimbilia alfajiri katika lango la wabunge kuingia ukumbini ili kuwataka watie saini azimio hilo la hila, kanuni za bunge zilisababisha mpango huo mzima uyeyuke papo hapo utadhani tonge la siagi lililotumbukizwa motoni.
Akitekeleza ushauri wa busara wa Kamati ya Wabunge Wote wa CCM, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Kikwete alifanya mabadiliko katika baraza hilo ilipofika Mei 7, 2012. Aliwapumzisha baadhi ya mawaziri huku wengine wakibadilishwa wizara na hata vinginevyo na hivyo kuzima hoja hiyo kwa hekima.
Lakini ilipopita miezi miwili tena baadaye, wabunge hao wa upinzani pamoja na wachache wa CCM wanaokuwa na chuki zao wenyewe wakaibuka na jambo jingine. Sasa wakataka Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Eliackim Maswi eti wafukuzwe.
Muhongo aliyekuwa ndiyo kwanza amemaliza mwezi mmoja tu katika wizara hiyo akiwa na wadhifa huo alijengewa tuhuma za majungu, wivu, hasira na chuki za maslahi ya kisiasa na hata kiuchumi na kuanza kushinikizwa aondoke.
Naishukuru serikali hasa Rais Kikwete kwa kusema “hatoki mtu yeyote”. Aligoma kwa namna zote kuwang’oa madarakani au kuwahamishia mahali pengine. Namshukuru kwa kutosikiliza majungu yaliyotengenezwa na wabunge hao wenye chuki zao kwa CCM na serikali yake.
Mbali na kutaka Dk. Kawambwa ang’olewe katika mpango huo wa sasa, wabunge hao pia wanapanga kuwang’oa Spika wa Bunge, Anne Makinda na Naibu wake, Job Ndugai kwa tuhuma za kusitisha hoja ya kutaka suala zima la gesi iliyoibua vurugu kubwa kule Mtwara kuwa lijadiliwe bungeni.
Baada ya awali Spika kusema kuwa angeunda Tume ya Bunge ili kwenda katika mkoa huo kupata ukweli, lakini alitangaza tena baadaye kwamba asingefanya hivyo kwa vile tayari Waziri Mkuu alikuwa amelishughulikia jambo hilo kwa namna zote na kupata suluhu yake.
Mbali na hayo, nani asiyejua ukweli kuwa wao ndio waliongoza uchochezi wote wa gesi ili kukidhi matakwa yao ya kutaka Tanzania isitawalike mwaka 2013? Nani hakumsikia kwa namna moja ama nyingine Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Wilbroad Slaa aliposema kazi hiyo imefanywa na chama chake, na kwamba itaendelea mpaka mwaka 2015?
Leo wanapong’ang’ania iundwe tume ya uchunguzi pamoja na kutaka kulijadili suala hilo bungeni wanadhani kuwa nani hajui lolote wala chochote? Kwa nini serikali ipoteze fedha kwa kuwalipa wabunge waliotarajiwa kuwemo katika kikundi hicho wakati tayari undani na ukweli wa vurugu hizo zote umeshapatikana?
Mgogoro wa Mtwara uliratibiwa na wapinzani haohao kutoka vyama vinane vya siasa ambavyo ni pamoja na NCCR – Mageuzi ya Mbatia, TLP ya Mrema na pia Chadema ya Tundu Lissu, halafu hivi leo wanajidai kule bungeni kwamba iundwe tume ya kuchunguza uchochezi wao utadhani hawahusiki.
Walifanya hivyo kwa kutaka mwakilishi wao ndani ya tume hiyo ambaye ilikuwa lazima awemo, akakutane na viongozi wa umoja wa vyama vyao waliokuwa wakiratibu moja kwa moja uchochezi wao katika mkoa huo, kisha akisharudi Dodoma aje awape mrejesho.
Walitaka awemo ili akakutane na Mwenyekiti wa Umoja wa Vyama hivyo wilayani Mtwara, Uledi Abdallah pamoja na Katibu wake, Saidi Kulaga na hivyo kupata undani na ukweli wa sakata lote ili ikiwezekana walitengenezee uongo mpya ama pengine wahamie mkoa mwingine.
Nahitimisha kwa kuuliza swali moja kuwa je; hivi wabunge hawa wenye kazi kubwa ya kuchochea uasi kwa serikali, kupotosha ukweli na kususia vikao vya bunge wana faida gani kwa taifa kama siyo laana?
Mwandishi wa makala hii ni Katibu Msaidizi, Idara ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa ya CCM. Anapatikana kwa Simu Na. 0659 220 220 na 0762 633 244
Na Charles Charles IJUMAA iliyopita, wabunge wote wa kambi ya upinzani katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania walioku... [Read More]
Lema anapiga marufuku
wananchi kupata habari?
o Heche naye aonyesha anavyotumiwa na Dk. Slaa
Na Charles Charles
MBUNGE wa Arusha Mjini kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Godbless Lema amewalisha kiapo wafuasi wake cha kuwapiga marufuku kununua baadhi ya magazeti, kutazama vituo viwili vya televisheni na kutosikiliza kituo kimoja cha redio nchini.
Lema aliyekuwa akiwahutubia wafuasi wake hao kwenye Uwanja wa Kituo cha Mabasi cha Nduruma mjini humo, Jumamosi iliyopita, alivuliwa ubunge na Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha Aprili 5, mwaka huu, kabla ya kurudishiwa na Mahakama ya Rufaa jijini Dar es Salaam, siku moja kabla ya hapo.
Katika hotuba yake hiyo, Lema aliwaambia wananchi waliokuwepo katika mkutano wake huo kwamba wasinunue magazeti ya UHURU, HABARI LEO, TAZAMA TANZANIA na JAMBO LEO, na kwamba wasiangalie kwa namna yoyote ile vipindi vinavyorushwa na Kituo cha Televisheni cha Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC1) pamoja na Star TV wala kusikiliza kituo cha Radio Five ya jijini Arusha.
Alisema kuwa magazeti hayo sambamba na vituo hivyo vitatu katika ujumla wake vimekuwa vikiisakama sana kihabari Chadema, jambo alilodai kwamba haviitakii mema isipokuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na adhabu yake iwe ni kususiwa kununuliwa, kuangaliwa na hata kusikilizwa kwa namna zote.
Sikutarajia kuwa mbunge na Mjumbe wa Kamati Kuu ya chama na hasa kinachodai siku zote kwamba kinapigania uhuru wa habari, uhuru wa mtu kushirikiana na watu wengine, uhuru wa kutoa maoni, haki ya kupata ujira wa haki pamoja na haki ya kumiliki mali ndiye anakuwa wa kwanza kuwanyima haki hizo zote wapiga kura wake.
Ibara ya 18(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 Toleo la 2005 inayoendelea kutumika sasa inaeleza ifuatavyo:
“Kila mtu anayo haki ya kupewa taarifa wakati wote kuhusu matukio mbalimbali muhimu kwa maisha na shughuli za wananchi, na pia kuhusu masuala muhimu kwa jamii” (mwisho wa kunukuu).
Akiwa Mbunge na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Lema alipaswa kuwa mstari wa mbele kwa juhudi na maarifa yake yote, kuhakikisha kwamba ibara hiyo ya Katiba ya nchi inaheshimiwa na kila Mtanzania, lakini inashangaza kuona badala ya kuitetea kwa nguvu zake zote, yeye ndiye anakuwa wa kwanza kuikiuka kwa kuwataka watu wavibague baadhi ya magazeti, redio na televisheni nchini ili wakose habari.
Ni ajabu kuona mbunge anakuwa na kinyongo na baadhi ya vyombo hivyo vya habari eti kwa sababu tu haviimbi utukufu wake kama vinavyofanya vile ‘vinavyomilikiwa’ kwa namna moja ama nyingine na chama chake, jambo ambalo ni ujinga kuvilazimisha vyote viwe kama midomo yake au kumsifu kila kwa kila neno analosema kinywani mwake hata kama halina faida yoyote kwa watu wengine, taifa letu, Afrika yetu au hata ulimwengu.
Ni ujinga kutaka eti magazeti yote, redio pamoja na vituo vyote vya televisheni nchini kila moja iwe inatangaza mambo anayoyataka mwenyewe au kuwaponda wengine, na kwamba kila anapowatukana wanachama, viongozi na wafuasi wa chama kilichopo madarakani ama serikali yake basi vyote vimuunge mkono katika hali anayoitaka yeye.
Bila ya kujali itikadi yake ya kisiasa na kuiona kuwa ni bora kuliko zote zilizobaki, Lema anapaswa aheshimu ukweli kwamba kila mtu ana haki ya kuwa na maoni na kueleza fikra zake kwa watu wengine, jambo ambalo linaelezwa vizuri katika Ibara ya 18(a) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Anapaswa akubali na kuheshimu ukweli kwamba kila mtu ana haki ya kuamini chama cha siasa anachokitaka yeye mwenyewe, ile ambayo imeelezwa katika Ibara ya 3(1) ya Katiba hiyo ya nchi inayosema ifuatavyo:
“Jamhuri ya Muungano ni nchi ya kidemokrasia na ya kijamaa, isiyokuwa na dini, (na) yenye kufuata mfumo wa vyama vingi vya siasa” (mwisho wa kunukuu).
Katika hali hiyo na hata vinginevyo, hatua iliyofanywa na Lema ya kuwalisha yamini wafuasi wake kuwa wasinunue magazeti ya UHURU, HABARI LEO, TAZAMA TANZANIA na JAMBO LEO, kutosikiliza kituo cha Radio Five wala kutoangalia Star TV na TBC1 ni ujinga uliovuka mpaka akilini.
Yeye mwenyewe anafahamu yamini yake kwa wafuasi wake siyo lolote wala chochote na hakuna yeyote anayeweza kuwa vyovyote pindi akienda kinyume chake.
Haiwezi kumdhuru yeyote hata iweje kwa sababu siyo Mungu wala taasisi ya kisheria. Ana mfano hai kuwa hata yamini aliyokula Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa kwa Mungu wake siku alipotunukiwa ushemasi na upadri alikuja kwenda kinyume chake, lakini bado hakufanywa chochote.
Alimwahidi Mungu kwamba angeishi kiseja katika maisha yake yote, lakini akashindwa na kufunga ndoa na mwanamke wakati akiwa Mtawa wa Kanisa Katoliki, yule aliyepata naye watoto wawili na hatimaye akawatelekeza mkoani Manyara.
Wote waliokula kiapo hicho mkutanoni siku hiyo kwamba hawatanunua kabisa magazeti hayo, hawataangalia vituo hivyo viwili vya televisheni wala kusikiliza kituo hicho cha redio hakuna hata mmoja ambaye kweli ataacha kwa kumhofia Lema isipokuwa kama pia ni mjinga wa kufikiri kichwani.
Pamoja na sababu nyingine, wengi waliapa kwa kuogopa macho ya watu ili kuepuka vipigo vya baadhi ya wafuasi wake ambao kuna wengine ni wendawazaimu vichwani kama yeye mwenyewe, lakini walipofika majumbani wakaendelea kuzingalia TV zote hizo zikiwemo taarifa zake za habari, na pia kuna wengine waliendelea kusikiliza Radio Five na kusoma magazeti yote hayo kwa namna moja ama nyingine.
Mbali na kuzuia uhuru wa kupewa taarifa za matukio ambayo ni muhimu kwa maisha na shughuli nyingine za watu, kiapo kilichotolewa na Lema kwa wafuasi wake pia kililenga kuzuia ajira kwa baadhi ya vijana wanaoishi, kutunza familia na kutoa huduma mbalimbali kwa wategemezi wao kwa kufanya biashara ya kuuza magazeti hayo bila ya kujali itikadi zao za kisiasa.
Hatua yoyote ya kuwalisha watu kiapo kwamba wasiyasome maana yake ni kutaka vijana hao washindwe kuwahudumia wake zao, waume zao, watoto wao, baba zao, mama zao, babu zao, bibi zao, watumishi wao wa ndani na hata kutoa msaada wowote kwa ndugu zao wengine na kadhalika.
Anataka wakose ajira ili pengine wawe wezi wa mifukoni, vibaka wa usiku, matapeli wa mjini, majambazi wanaoua watu, makahaba wanaouza miili yao kwa kutoa mapenzi ya kawaida au kinyume cha maumbile yao na kufanya uhalifu mwingine.
Badala ya kuzungumzia ujinga na kuwalisha watu viapo vya kiwendawazimu mkutanoni, Lema alipaswa angalau ajibu tuhuma za jinai zinazoelekezwa kwake hivi sasa na baadhi ya vyombo vya habari zikiwemo za wizi wa kuaminika, ufisadi wa mali na misaada ya fedha na mali nyingine kwa chama chake na kutokuwa mwaminifu akiwa kiongozi mwandamizi wa Chadema na mbunge wa kuchaguliwa jimboni.
Likiandika katika toleo lake namba 220 la Jumanne Desemba 11 – 17, 2012, gazeti la FAHAMU litolewalo mara moja kila wiki lilidai kwamba Lema anatuhumiwa kutafuna fedha zilizochangwa na wanachama, viongozi na wafuasi wa Chadema ili kugharamia maandamano na mikutano ya Vuguvugu la Mabadiliko (M4C) hata kama inafanyika kwa vurugu, fujo na umwagaji wa damu.
Alipaswa aitumie nafasi hiyo kuwaambia wapiga kura wake endapo anahusika au hahusiki kwa namna moja ama nyingine na tuhuma za ‘kuingia mitini’ na pikipiki aina ya Kawasaki iliyotolewa msaada na wafadhili wa Chadema.
Alipaswa aseme ni wapi alikolipeleka trekta alilokabidhiwa na wafadhili wa Chadema ili kuwasaidia wajane kwenye mashamba yao, pembejeo ya kilimo aliyopewa pindi tu baada ya kuapishwa kwake na kuwa mbunge mpya wa Arusha Mjini mwaka 2010.
Alipaswa awaambie ni wapi lilikokwenda na ilikuwaje, hatua ambayo ingewezesha wajue endapo linafanya kazi aliyoelekezwa na wafadhili waliompa kwa ajili ya wajane hao, kina mama ambao kuna wengine waliachiwa watoto ama pengine wajukuu baada ya kufiwa na wapendwa wao.
Alipaswa awaeleze kuhusu ukweli wa tuhuma dhidi yake kwamba amekuwa akichangisha fedha kwa ajili ya kuwasaidia wajane na watoto waliofiwa na wazazi wao na kuzitafuna zote, na kwamba anatumia propaganda zinazolenga kuwadhoofisha baadhi ya wanachama na viongozi wenzake wa Chadema.
Alipaswa ajibu tuhuma kwamba amekuwa akichangisha mamilioni ya fedha kutoka kwa matajiri wa Arusha akidai kuwa yeye ni Mwenyekiti wa Taifa wa M4C, na kwamba hata fedha zilizochangiwa familia za marehemu waliopigwa risasi siku ya maandamano ya vurugu za Chadema za Januari 5, 2011 hadi sasa hazijawafikia walengwa.
Alipaswa azungumzie tuhuma kwamba amekuwa akikusanya fedha nyingi anazodai kuwa za kusomeshea watoto kupitia Shirika la Arusha Development Fund (ARDF), lakini zote au nyingi kati yake hazifahamiki ni wapi zinakokwenda.
Alipaswa awaambie kuhusu madai kwamba alitumia shirika hilo pia kuombea kiwanja cha ujenzi wa hospitali ya umma, gari la wagonjwa na vifaa vingine vya huduma kwa ajili ya jimbo hilo la Arusha Mjini.
Kukimbilia kuwatisha watu kwa yamini kuwa wasinunue magazeti fulani, wasikilize redio fulani au wasiangalie vituo fulani vya televisheni ni harakati za kijinga au wendawazimu wa kufikiri ambao ni ajabu zaidi unapofanywa na Mbunge, Mjumbe wa Kamati Kuu ya chama cha siasa na hata kiongozi mwingine yeyote wa umma.
Mbali na Lema, Mwenyekiti wa Taifa wa Baraza la Vijana wa Chadema (Bavicha), John Heche alinikumbusha pia tuhuma zake alipodai kuwa chama hicho kinajipanga kumpeleka Ikulu Katibu Mkuu wake, Dk. Willibrod Slaa ifikapo mwaka 2015.
Akiandika katika baadhi ya mitandao ya kijamii wiki iliyopita na baadaye kulithibitishia gazeti dada la MZALENDO, Makamu Mwenyekiti wa Bavicha, Juliana Shonza alieleza kwa kina namna Heche anavyotumiwa na Dk. Slaa ili kuligawa na kulivuruga baraza hilo la vijana wa Chadema kwa ajili ya maslahi yao binafsi.
Katika kufanya hivyo, Shonza alidai kuwa Dk. Slaa ameidhinisha Heche alipwe mshahara wa shilingi 700,000 kila mwezi kutokana na ruzuku inayotolewa na serikali kwa Chadema, jambo linalokwenda kinyume cha Katiba ya chama hicho kwa sababu anayepaswa kulipwa mshahara namna hiyo ni Katibu Mkuu wa Bavicha na siyo Mwenyekiti wake.
“Kumlipa mshahara Heche ni kuligawa Baraza la Vijana kwa sababu ni ukiukwaji wa Katiba ya chama…Ni wazi (kwamba) anamlipa fadhila kwa yale aliyofanya ya kuendesha baraza kwa misingi ya kauli za Katibu Mkuu”, anasema Shonza katika taarifa yake hiyo na kumshutumu kwa kuingiza ukanda na ukabila ndani ya Chadema.
Mbali na tuhuma za mshahara, Shonza pia anasema Dk. Slaa aliidhinisha kuwa Heche alipwe shilingi 2,000,000 za pango la nyumba aliyotafutiwa na Chadema baada ya kuwa Mwenyekiti wa Bavicha.
Hatua hiyo inatajwa kuwa inawabagua viongozi wa Bavicha kimatabaka ambapo Makamu Mwenyekiti, Katibu Mkuu na wengine wote hawana umuhimu, na kwamba hawaonekani kuwa lolote wala chochote katika chama hicho na huenda hawana faida yoyote kisiasa.
Mlolongo wa tuhuma hizo pia unagusia gari aina ya Nissan Patrol lenye rangi nyekundu linalodaiwa kutolewa kwa Bavicha na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema (Tanzania Bara), lakini katika hali ya ufisadi, Makamu Mwenyekiti huyo anasema lilichukuliwa na Heche anayelitumia kwa shughuli zake mwenyewe huku dereva wake akitajwa kuwa ni mdogo wake.
Katika hali hiyo, sishangai hata kidogo kumuona kijana huyo akitangaza mkutanoni kuwa Dk. Slaa ndiye mgombea urais wa Chadema mwaka 2015 kinyume cha Katiba, kanuni na taratibu nyingine za kawaida za kichama.
Anafanya hivyo ili kuthibitisha tuhuma za Shonza dhidi yake kuwa kuna mchezo ‘mchafu’ ambao unaendelea kati yake na Dk. Slaa huku viongozi wengine wa Bavicha wakitengwa.
Wanalipana fadhila kutokana na kazi wanazopeana kwa ajili ya maslahi yao na siyo kwa faida ya chama wala wanachama, viongozi au wafuasi wa Chadema kama taasisi ila kama kampuni binafsi au Shirika Lisilokuwa la Kiserikali (NGO) linalomilikiwa na familia ama watu wenye malengo wanayoyajua wenyewe.
Bila ya kujali kuwa ni ndani ya Chadema na hata vinginevyo sehemu zote duniani, hakuna Mwenyekiti awe wa NGO, chama cha siasa wala taasisi yoyote na hata vitengo vyake anayelipiwa pango la nyumba au kupewa mshahara ila wote wanapata posho za vikao peke yake, safari ama za uwajibikaji pale wanapokuwa katika kazi zinazotajwa na Katiba za taasisi zao.
Hawalipiwi kodi iwe ya pango ama nyingine yoyote wala kupewa mishahara kwa vile kazi zote zinazohusu uenyekiti haziwi za ajira isipokuwa kujitolea, hivyo haiwezekani Heche afanyiwe kinyume chake endapo siyo rushwa ya kisiasa anayopewa ili naye pia ‘amlinde’, amtetee au kumuunga mkono kwa nguvu zake zote Dk. Slaa.
Aliposema kuwa anakusudia kugombea urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 kama chama chake kitampitisha, Zitto alikemewa kwa nguvu nyingi na viongozi wake waliodai kwamba muda wa kutangaza jambo hilo bado haujafika na hata kukaribia pekee.
Alikaripiwa na mwasisi wa Chadema ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taifa Mstaafu wa chama hicho, Mzee Edwin Mtei na hata Mwenyekiti wa Taifa sasa, Freeman Mbowe na pia Dk. Slaa kwa ulimi wake mwenyewe.
Kinachonishangaza sana ni ukweli kwamba Zitto hakutangaza kuwa yeye ndiye mgombea urais wa chama hicho wakati huo, badala yake alichosema ni kwamba ataomba ridhaa ya kufanya hivyo kwa kuzingatia Katiba ya Chadema, kisha akaomba Mungu akubaliwe na wenzake ili akiipata nafasi hiyo aitumie vizuri kuiongoza Tanzania kwa jinsi inavyopaswa.
Tofauti na kijana huyo ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini kwa muhula wa pili sasa, Heche yeye ametangaza rasmi kuwa katika uchaguzi huo mkuu ujao, mgombea urais wa Chadema atakuwa ni babu huyo wa Karatu aliyetelekeza mkewe na watoto wake.
Amefanya hivyo kwa sababu huenda ndiyo makubaliano waliyofikia kwamba yeye alipiwe pango la nyumba, apewe mshahara huo mnono kinyume cha Katiba ya Chadema na ahodhi gari lililotolewa na Zitto kwa ajili ya Bavicha, lakini naye katika upande wa pili apambane kikamilifu kuhakikisha kuwa Dk. Slaa ndiye anagombea urais mwaka 2015.
Wamelishana yamini kwamba kila mmoja amtumikie mwenzie, hivyo haishangazi kuwa Heche aliamua kumtangaza hadharani mkutanoni babu huyo wa Karatu kugombea nafasi hiyo katika uchaguzi huo mkuu wa rais, wabunge na madiwani; halafu haijalishi kama alikwenda kinyume cha Katiba, kanuni na taratibu nyingine za Chadema.
Alifanya hivyo sambamba na Lema ambaye aliwalisha yamini wafuasi wake ili wayasusie magazeti yale, televisheni zile pamoja na redio ile kwa sababu wote ninadhani kuwa akili zao za kisiasa ni za kishamba, kilimbukeni na ovyo, na kwamba inawezekana upeo wao wa kupembua mambo ya utawala na uongozi wa umma ni mdogo sana.
Ndiyo maana licha ya kuwa kwao wote ni Wajumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, lakini akili zao bado ni sawa na za watoto wa chekechea, hatua inayosababisha waseme chochote, wakati wowote na mahali popote bila ya kujali ama kufahamu kwamba athari zake kwao au kwa umma ni kubwa kupindukia!
Mwandishi wa makala hii ni Katibu Msaidizi, Idara ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa ya CCM. Anapatikana kwa e-mail: mimi.mimi011@yahoo.com
Lema anapiga marufuku wananchi kupata habari? o Heche naye aonyesha anavyotumiwa na Dk. Slaa Na Charles Charles MBUNGE wa Aru... [Read More]